MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Shinyanga,
Khamis Mgeja amesema chama hicho kimeacha misingi yake na sasa kimegeuka kuwa
ya kampuni.
Mbali na hilo, pia alimpiga kijembe mgombea urais kupitia
CCM, Dk. John Magufuli akimfananisha na dereva ambaye hajaweza kuendesha gari
vizuri ‘learner’ akimaanisha kuwa hana uwezo wa kukiongoza chama hicho.
Mgeja alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam wakati
akitangaza kukihama chama hicho na kujiunga na Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema), huku akiambatana na aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa
Dar es Salaam, John Guninita ambaye na yeye amejiunga na chama hicho kikuu cha
upinzani nchini.
Mwanasiasa huyo mkongwe aliyepata kushika nyadhifa
mbalimbali ndani ya CCM, alisema ametumika ndani ya chama hicho kwa muda mrefu
huku akishiriki kurekebisha kasoro mbalimbali zilizojitokeza lakini sasa imefika
mwisho.
“Pamoja na kuzirekebisha kasoro zilizojitokeza mara kadhaa lakini
kila jambo lina mwisho wake na kurekebisha mambo hayo nayo inafika mwisho.
“Chama sasa kimekuwa cha BMW yaani cha baba, mama na
watoto. Kwa maana hiyo chama kimekuwa cha kampuni au familia ndio maana maoni
ya wanachama na wananchi yanapuuzwa,”alisema.
Mgeja ambaye pia aliongozana na makada wengine wa chama
hicho, alisema yeye pamoja na wenyeviti takribani 23, wajumbe wa Halmashauri
Kuu (NEC) pamoja na baadhi ya wabunge waliona mabadiliko yanahitajika ndani ya
CCM.
“Matatizo ndani ya chama ni makubwa tunastahili tupate
dereva fundi kwa sababu sisi tuliokitumikia chama tunakifahamu hapa tulipofika
hivyo kinahitaji ukarabati mkubwa na tukashawishika kuwa Lowassa anaweza.
“Lakini kwa bahati mbaya mawazo ya wanachama, wananchi
mwenyekiti wetu ameyapuuza. Nilikuwa navuta subira angekuwa muungwana
angezungumza na kuomba radhi kwa aliyoyafanya kwani hayavulimiliki. Anakuja
kwenye vikao vizito na akiwa na majina matano mfukoni.
“Tukamwuliza
atusomee sifa za hao wagombea watano lakini akafanya ubabe, akatengeneza nguvu
kubwa, polisi wakazunguka lile jengo wakiwa na mabomu, farasi, gari ya maji ya
washasha na hata ndani ya ukumbi polisi walikwepo wakiwa na mabomu.
“Nilimwuliza mwenyekiti kwamba leo tuko Burundi…tunawalalamikia
kina Nkurunziza kumbe tunao wengi Tanzania. Tulipekuliwa na vijana wadogo
wanakutana na hirizi zetu.
“Taswira ya chama imeondoka. Mliona kina Emmanuel Nchimbi
walitoka wale hawakuwa wajinga waliona kasoro kubwa imefanyika,”alisema.
Alisema chama kimekuwa si kile cha wakati wa Mwalimu
Nyerere kimejaa chuki, rushwa, fitna, kimepoteza mwelekeo na kwamba nguvu
zilizotumika wakati wa kumpata mgombea urais ilikuwa hatari sana.
“Chama kilikuwa kinahitaji dereva fundi, lakini sasa
kimekabidhiwa kwa Magufuli ambaye ni dereva leaner, hajawahi hata kuwa balozi
wa nyumba kumi hata mimi hanifikii nusu, nilitegemea mwenyekiti wa chama
angewaomba radhi wanachama lakini ameshindwa.
“Mwenyekiti
anakiacha chama vipande anaachaje kumweka Mwandosya kweli anazidiwa sifa na
January Makamba, hata waziri mkuu wake ameshindwa kumwamini huku jana yake
akimpongeza kuwa ni jembe lake.
“Hata Sitta wakati
ule wa spika alijitahidi ajibadilishe ikashindikana, sasa amemtumia bunge la
katiba naye kachinjiwa mbali, Tyson, Sumaye wote wamechinjiwa mbali halafu
anamuweka naibu waziri,”alisema.
Alisema kutokana na hayo ameamua kujiunga na Chadema kwenda
kuongeza mapambano.
“Kwanza nimuenzi
Mwalimu Julius Nyerere aliposema kwamba watu wakiyataka mabadiliko wakayakosa
ndani ya CCM wayatafute nje ya chama hiki. Sasa mimi ninamuenzi kwa moyo
mkunjufu, nimeamua kuchana na CCM.
“Kwa heshima kabisa bila kumung’unya maneno natamka
kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) tukapambane huko,”alisema
Mgeja huku akikunja ngumi na kusema ‘peoples’.
Pia aliwataka makada wa chama chake ambao wamekuwa na tabia
ya kurusha vijembe na kumchafua Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa
wakapambane kwenye midahalo kwa hoja.
“Kama wao ni wanaume sasa twende kwenye midahalo wasimung’unye
maneno kusema ukweli. Na haya niliyoyafanya mimi na wenzangu ndiyo maamuzi
magumu,”alisema.
GUNINITA
Kwa upande wake aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es
Salaam, John Guninita alisema amezaliwa akiwa CCM na kwamba alikitumikia chama
hicho kwa muda wa miaka 35, lakini kutokana na kukiukwa kwa misingi ameamua
kuhama.
Alisema ni dhahiri kuwa vijana wadogo ambao wanawatukana
viongozi wenye umri zaidi ya baba zao, wametumwa chama.
“Haiwezekani kijana mdogo anamtukana viongozi wakubwa huku
chama kikikaa kimya na mwishoni kupata uongozi kwa utaratibu wa uyoga uyoga,
sijui laana hii wataipeleka wapi,”alihoji Guninita.
Alisema CCM kilipofikia sasa kinakufa kama ilivyokuwa kwa
chama cha KANU cha Kenya na UNIP ya nchini Zambia.
“Binadamu anapozaliwa anakuwa na malengo yake, inafika
unaugua na kufa na sasa CCM kinaugua na majibu ya dokta ni lazima yaonyeshe
kuwa kimekufa,”alisema.
Alisema makada wa chama hicho ambao wamekuwa wakimshambulia
Lowassa watashughulikanao kwenye kampeni na kwamba waziri mkuu huyo zamani akae
kimya kwa kuwa yeye anawamudu.
“Edward atuachie sisi tuna uwezo wa kuwamudu hawa makuruta
wa siasa wa aina ya Nape,”alisema Guninita.
Mwisho.