Thursday, May 28, 2015

HEDHI SALAMA KWA MWANAFUNZI IMESISITIZWA



WIZARA ya Elimu kwa kushirikiana na wadau wataendelea kusimamia sera inayotaka kuondoa vikwazo vyote vinavyomsababisha mwanafunzi kutohudhuria masomo.
Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya Hedhi duniani leo jijini Dar es Salaam, Afisa Elimu Mkuu wa Wizara ya Elimu na mafunzo ya Ufundi, Madina Kemilembe alisema kukosekana kwa miundombinu rafiki mashuleni kunasababisha wanafunzi kukosa masomo.
Alisema ukosefu wa mazingira bora kama vyoo, maji safi na salama, sabuni ya kunawia pamoja chumba cha kubadilishia nguo hasa kwa watoto wakike wanapokuwa hedhi mashuleni kunasababisha utoro mashuleni.
“Nawashukuru wadau Water Aid, Shirika la maendeleo la Uholanzi(SNV), Kasole Secret pamoja na wengine kwa kuisaidia serikali kuandaa mazingira rafiki kwa watoto wetu kwa kuwajengea vyumba vya kubadilishia na kuwapelekea maji safi na upatikanaji wa pedi kwa baadhi ya shule,” alisema Kemilembe.
Alisema kutokana na ukosefu wa pedi baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakitumia vitambaa visivyosalama na wanapovifua vinaanikwa chini ya godoro hivyo kusababisha magonjwa mbalimbali kama fangasi kwa kutokauka vizuri.
Alisema ifikie wakati jamii ivunje ukimya kwa kuongelea suala la hedhi kwa uwazi kwani linamyima mtoto wa kike masomo hasa kipindi anapokuwa hedhi.
“Elimu itolewe kwa wazazi pamoja na wanafunzi wote wa kike na wa kiume ili kuondoa unyanyapaa ili kuboresha mazingira ya kusoma kwa mtoto wa kike,” alisema Kemilembe.
Kwa upande wake Meneja wa Mradi wa Girls in control menstral hygien management kutoka Shirika la Maendeleo Uholanzi, Rozalia Mushi alisema mradi wake utaendelea kuangalia jinsi ya kumsaidia mtoto wa kike aliyeko mashuleni ili kumuongeza ufaulu katika masomo yake.
“Mtoto wa kike anakosa vipindi 450 kwa mwaka anapokuwa katika hedhi kitu ambacho kinampunguzia ufaulu katika masomo yake kutokana na kutokujiamini na unyanyapaa anapokuwa darasani,” alisema Mushi.
Alisema walimu pia walikuwa wakitoroka kufundisha kutokana na kuwa katika hali hiyo hivyo waliamua kujenga vyumba vya kubadilishia katika shule mbalimbali.
Nae Mkurugenzi wa Water Aid, Ibrahimu Kabole alisema kuna uelewa mdogo pamoja na mila potofu zinazofanya jambo la hedhi kuonekana ni la aibu.
“Asilimia 40 ya wanafunzi wa kike hutoroka shule kutokana na kuzomewa,kunyanyapaliwa pamoja na kukosa mazingira rafiki wanapokuwa kwenye hedhi,” alisema Kabole.
Alisema jamii ipewe uwezo kujua jambo hilo na liongelewe kwa uwazi ili kuwajengea mazingira bora ya kusoma.
Siku ya hedhi duniani kwa mara ya kwanza imeadhimishwa nchini kwa maandamano ya wanafunzi wa kike kutokea Wizara ya Elimu na mafunzo ya ufundi na kumalizikia viwanja vya mnazi mmoja jijini Dar es Salaam.

Sunday, May 24, 2015

UDSM WALIA NA LUBUVA



 WANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Dar es Salam (UDSM), wameiomba serikali kuhakikisha inaweka mfumo madhubuti wa kuandikisha wanafunzi kwenye daftari la Kudumu la Wapiga kura ili haki yao kikatiba itekelezeke.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mikopo wa Serikali ya Wanafunzi (DARUSO), Shitindi Venance alisema, hadi sasa hakuna utaratibu wowote wa wao kuandikishwa katika daftari hilo jambo ambalo linaonyesha kuwanyima haki yao ya msingi.
“Sisi kama wanavyuo na kila aliyepo chuoni hapa ni mtu mzima ametimiza miaka 18, lakini kwa utaratibu uliopo inaonyesha dhahiri wanataka kutunyima haki yetu ya kuwachangua viongozi tunaoona wataleta mabadiliko nchini.
“Tumeamua kutoa ombi hili baada ya kuona utaratibu wa kuandikisha ukiendelea kufanyika katika majimbo yetu wakati sisi tupo chuoni tukiendelea na masomo na hadi sasa hatujapewa utaratibu wa kuandikishwa katika vyuo,” alisema Venance.
Venance alisema ni vyema serikali ikaona haja ya kufungua matawi katika vyuo mbalimbali nchini na kuandikisha wanafunzi katika daftari hilo ili wapate haki ya kumchagua kiongozi wanayemhitaji.
Alisema inasikitisha sana wao kukosa haki hiyo hadi sasa kwani vijana ndiyo wenye kuleta changamoto ya kupata viongozi wenye manufaa ambao wako tayari kuleta mageuzi ya kiuchumi katika majimbo yao.
“Tunaomba Serikali iliangalie kwa umakini suala hili kwani sisi ndiyo wenye uwezo wa kuwaelimisha wananchi vijijini kiongozi yupi anafaa hasa ukizingatia maeneo hayo baadhi yao hawana uelewa wa yupi anafaa kuwa kiongozi bora,” alisema Venance.
Alisema mzalendo wa kweli anaheshimika kwa elimu yake na si kumfundisha mtu uzalendo kwa kumpeleka jeshini ambapo aliiomba serikali kuwaelewa katika hilo

VIJANA WASEMA RUFIJI KURA YA MAONI PATACHIMBIKA



VIJANA wa wilaya ya Rufiji wameamua kutoa elimu ya mpiga kura kwa wananchi hasa kipindi cha kura za maoni ili kujenga uelewa kwa wananchi hao .
Wakizungumza jijini Dar es Salaam kwa nyakati tofauti vijana hao walisema wameamua kutoa elimu hiyo ili kuubadilisha mfumo uliopo hasa ndani ya Chama cha Mapinduzi(Ccm) ambao unawanyima haki ya kuchagua kiongozi bora.
Mmoja kati ya vijana hao,Juma Kiholobele alisema mfumo uliopo unasababisha watu wenye fedha kuwa ndio wenye haki ya kuwa viongozi.
“Tunaenda kuwaeleza wenzetu wasiojua kabisa, wanaojua kidogo na wanaojua sana kuwa lazima mfumo urudi kama ulivyoasisiwa ambapo tulikuwa tukiangalia uwezo wa mtu katika uongozi,” alisema Kiholobele.
Alisema mfumo wa kugawa fedha kipindi cha uchaguzi unawanyima wananchi haki ya kusikiliza sera na malengo ya mgombea.
“Tutapambana na mfumo uliopo ambao fedha zinatumika kama raslimali ya kupata uongozi ambapo mamlaka yanabaki kwenye familia chache zenye kipato,” alisema Kiholobele.
Alisema mfumo huo unasababisha watu wenye fedha kuwa wizi kwa kuwa itabidi warudishe mitaji yao(fedha) waliyotoa kipindi cha uchaguzi hivyo kurudisha maendeleo ya nchi nyuma.
Alisema mabadiliko yapatikane ndani ya CCM ikishindikana watayatafuta nje.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Uvccm wilayani Rufiji, Shabani Matwebe alisema atahakikisha wanachama, viongozi na mashabiki wa CCM wanafuata katiba na kanuni za chama hicho katika kupata wagombea.
“Vijana tuone kama tumechelewa kuubadili mfumo huu kwani katiba na kanuni za CCM katika kupata wagombea tunazijua na ni lazima sasa tuzitumie na si kusubiri nani ana fedha nyingi mwaka huu,” alisema Matwebe.
Alisema kura za maoni mwaka huu ndani ya chama hicho zitakuwa za ushindani kama CHADEMA na CCM kutokana na watu kuelimika kupitia wao.
Nae mwanachama wa ccm, Jamvi Magawa alisema rushwa ndani ya CCM ndiyo chanzo cha tatizo la ukosefu wa maadili ndani ya chama hicho.
“Kwa sababu ya rushwa tumeendelea kuonewa na kunyanyaswa kwani hatuna mamlaka ya kumuuliza kiongozi ambae tulimchagua kwa wingi wa fedha zake kwa sababu tulikula 15,000 zake mwaka 2010,” alisema Magawa.
Alisema viongozi wanapokuwa vipofu kuona matatizo ya wananchi wao, wananchi watakuwa viziwi hawatawasikiliza viongozi wao.
                       





  
 

Wednesday, May 20, 2015

CHUO KIKUU DAR ES SALAAM (UDSM) WAMALIZA MGOMO



MGOMO wa wanafunzi wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), umemalizika na wanafunzi wote wameingia darasani na kuendelea na masomo kama kawaida baada ya Bodi ya Mikopo kuwaingizia fedha zao za kujikimu walizokuwa wamecheleweshewa kwa mujibu wa mikataba yao.
Akizungumza na FICHUA jana Waziri wa Mikopo  wa Serikali ya wanafunzi wa chuo hicho(DARUSO), Shitindi Venance alisema fedha walizokuwa wamecheleweshewa na Bodi ya mikopo(HESLB) ziliingizwa juzi jioni hivyo kumaliza kwa mgomo huo .
Alisema wanafunzi walikuwa wakiidai Bodi hiyo jumla ya shilingi bilioni 2.8 ambazo ni fedha za kujikimu kwa wanafunzi wanafunzi 6,120   kama inavyoainishwa kwenye mikataba yao na Bodi hiyo.
Alisema waliingia mkataba na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kuwa kila baada ya wiki nane watakuwa wanaingiziwa Sh 450,000 kwa ajili ya kujikimu mpaka mwishoni mwa wiki walikuwa hawajaingiziwa fedha hizo na kuwasababishia maisha kuwa magumu zaidi.
Alisema Serikali iache urasimu pamoja na kufanya kazi kwa mazoea kwa kusubiri shinikizo la migomo ndipo watekeleze majukumu yao.
“Tumekuwa tukisoma kwa shida kwa muda mrefu ambapo hata mwaka jana tulienda kufanya mafunzo kwa vitendo(field attachment) bila kulipwa fedha hadi tuliporejea,” alisema Venance.
Alisema Serikali inawafundisha vibaya kwani bila ya kuiadhibu kwa migomo na mashinikizo haitekelezi jambo kitu ambacho kinajenga taswira mbaya kwa jamii.
“Mwaka huu tunatangaza mapema kuwa kama fedha za kwenda kwenye mafunzo kwa vitendo(field) hazitakuwepo nasi hatutaenda,” alisema Venanc

Aidha alisema viongozi wengi walioko madarakani wanatumia vibaya nyazifa na fedha zao kuwalaghai wanafunzi wa kike nao kwa shida walizonazo wanajikuta wakiingia kwenye mitego hiyo.
“Tunawaona wanavyokuja na mashangingi yao kuwalaghai dada zetu huku hawawatekelezei madai yao wawalipe kwa wakati ili wasije wakaingia vishawishini,” alisema Venance.
Alisema anamkumbusha Waziri Mkuu Mizengo Pinda kauli yake aliyoitoa mwaka 2010 kuwa fedha za kujikimu zitakuwa zinapanda kila baada ya miaka mitatu kwani toka kipindi hicho mpaka sasa haijawahi kupanda.
“Tangu Waziri Mkuu aliposema kuwa watakuwa wanafanya tathmini na kupandisha fedha za kujikimu mpaka leo haijawahi kupanda japo gharama za maisha zinapanda kila siku,” alisema
Alipotafutwa, Msemaji wa Bodi ya Mikopo, Cosmas Mwaisobwa alisema madai ya wanafunzi wa vyuo vyote yameanza kushughulikiwa kwa kuanza na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

JESHI LA POLISI LAWAMANI KUWADHARIRISHA WANACHAMA CUF





TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), imetoa ripoti yake ya uchunguzi dhidi ya tuhuma kwa Jeshi la Polisi za kuwapiga na kuwadhalilisha viongozi na wafuasi wa Chama cha Wananchi (CUF), na kusema jeshi hilo lilitumia nguvu kupita kiasi na kuwadhalilisha wanawake wawili wa chama hicho.
Akitoa ripoti hiyo jana jijini Dar es Salaam kwa waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Bahame Nyanduga alisema pia jeshi hilo lilikiuka misingi ya Utawala Bora kwa wana CUF  katika tukio lililotokea eneo la Mtoni Mtongani wakati wanachama hao wakienda kuahirisha mkutano wao Mbagala Zakhem.
Nyanduga alisema tukio hilo la ukiukwaji wa  haki za binadamu lilitokea Januari 27,mwaka huu ambapo taarifa zilionyesha kuwa polisi hao waliwapiga na kuwakamata wananchi waliokuwa kwenye msafara wa Mwenyekiti wa CUF, Ibrahim Lipumba.
Alisema mambo yaliyobainika katika uchunguzi huo ni polisi kutumia nguvu kupita kiasi na kusababisha majeraha kwa viongozi wa CUF, kuathiri baadhi ya raia maeneo ya jirani na kukiuka misingi ya utawala bora kwa kutokuheshimu haki za binadamu.
“Tukio lile tume yetu pia ilibaini lilikuwa na udhalilishaji dhidi ya wanawake wawili wa CUF wakati wakikamatwa na kupelekwa mahabusu gereza la Segerea,”alisema Nyanduga.
Alisema kutokana na uchunguzi huo na matokeo ya ripoti hiyo tume imetoa mapendekezo kwa taasisi mbalimbali za serikali na vyama vya siasa kwa jeshi la polisi.
Alisema miongoni mwa mapendekezo hayo ni pamoja na kuzingatia kanuni, sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku, kutoa mafunzo kwa askari wake wanaoratibu shughuli za maandamano ya raia au vyama vya siasa.
Mengine ni kuhakikisha askari na maafisa wake wanapatiwa mafunzo ya mara kwa mara yahusuyo haki za binadamu na misingi ya utawala bora.
 pia katika operesheni zake lifuate utaratibu na kanuni za jeshi kwa kuzingatia jinsia za watumiwa na askari wanao washughulikia.
Wakati huohuo, Tume imetoa angalizo kwa polisi kuzingatia uhuru wa vyombo vya habari wakati wa utekelezaji wa operesheni zake na jeshi la Magereza lisitishe mara moja kufanya upekuzi wa watuhumiwa na kuepuka udhalilishaji wa heshima na utu wa binadamu.
Pia tume hiyo imekitaka chama cha CUF kutafuta namna ya kuboresha mahusiano na polisi ili kuepuka mivutano isiyo na tija katika shughuli za kisiasa, kuepusha vurugu na kulinda haki za binadamu.
“CUF  ilikiri kumiliki kikundi cha ulinzi cha Blue Guard hivyo tunakiomba kuzingatia katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inayozuia chama cha siasa kuwa na  kikundi cha mtazamo wa aina hiyo.