Monday, January 4, 2016

WASICHANA WATATU KUJENGEWA UWEZO



WASICHANA watatu kati ya 26 wamechaguliwa kuiwakilisha Tanzania katika mafunzo ya kuwajengea uwezo yanayoshirikisha mataifa mbalimbali duniani.
Mafunzo hayo yanayotolewa kupitia programu ya kubadilishana mabinti walioko katika vyama vya skauti wanawake duniani, yanashirikisha nchi za Tanzania, Rwanda, Afrika Kusini, Madagascar na Kenya.
Wasichana hao na nchi wanazokwenda ni Rose Mwambeta (Rwanda), Happines Mshana (Madagascar) na Mwaka Rashidi (Afrika Kusini).
Akizungumza jana wakati wa kuwakabidhi bendera na kuwaaga wasichana hao, Kamishna wa Tanzania Girl Guide, Symphrosa Hangi, alisema wasichana hao watakaa katika nchi hizo kwa miezi sita huku wakijifunza mambo mbalimbali.
“Nasisi pia tutawapokea wasichana watatu kutoka nchi hizo ambao watakaa hapa kwetu kwa miezi sita, kupitia kwao tutajifunza waliyokuwa wanayafanya na wao watajifunza mambo tunayoyafanya sisi,” alisema Hangi.
Alisema mchakato wa kuwapata wasichana hao ulitangazwa kwenye vyombo vya habari ambapo walijitokeza 26 na kuchujwa kisha wakapatikana watatu waliokidhi vigezo. Vigezo ni kuwa na umri kati ya miaka 18-25 na elimu ya kiwango cha stashahada.
Naye Mratibu wa Miradi wa Tanzania Girl Guide, Agnes Fivawo, alisema mambo watakayojifunza wasichana hao ni pamoja na utawala, ukufunzi na ujasiriamali.
“Tunabadilishana mabinti kutoka nchi moja kwenda nyingine ili waweze kujifunza mambo ya girl guide kwani yatawasaidia kukua kiakili, kujitegemea na hivyo kufanya mambo yao wenyewe,” alisema Fivawo.
Alisema wakiwa huko wasichana hao watapangiwa nyumba za kuishi na watakuwa wakilipwa posho ya kujikimu kila mwezi.

No comments:

Post a Comment