Wednesday, May 20, 2015

CHUO KIKUU DAR ES SALAAM (UDSM) WAMALIZA MGOMO



MGOMO wa wanafunzi wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), umemalizika na wanafunzi wote wameingia darasani na kuendelea na masomo kama kawaida baada ya Bodi ya Mikopo kuwaingizia fedha zao za kujikimu walizokuwa wamecheleweshewa kwa mujibu wa mikataba yao.
Akizungumza na FICHUA jana Waziri wa Mikopo  wa Serikali ya wanafunzi wa chuo hicho(DARUSO), Shitindi Venance alisema fedha walizokuwa wamecheleweshewa na Bodi ya mikopo(HESLB) ziliingizwa juzi jioni hivyo kumaliza kwa mgomo huo .
Alisema wanafunzi walikuwa wakiidai Bodi hiyo jumla ya shilingi bilioni 2.8 ambazo ni fedha za kujikimu kwa wanafunzi wanafunzi 6,120   kama inavyoainishwa kwenye mikataba yao na Bodi hiyo.
Alisema waliingia mkataba na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kuwa kila baada ya wiki nane watakuwa wanaingiziwa Sh 450,000 kwa ajili ya kujikimu mpaka mwishoni mwa wiki walikuwa hawajaingiziwa fedha hizo na kuwasababishia maisha kuwa magumu zaidi.
Alisema Serikali iache urasimu pamoja na kufanya kazi kwa mazoea kwa kusubiri shinikizo la migomo ndipo watekeleze majukumu yao.
“Tumekuwa tukisoma kwa shida kwa muda mrefu ambapo hata mwaka jana tulienda kufanya mafunzo kwa vitendo(field attachment) bila kulipwa fedha hadi tuliporejea,” alisema Venance.
Alisema Serikali inawafundisha vibaya kwani bila ya kuiadhibu kwa migomo na mashinikizo haitekelezi jambo kitu ambacho kinajenga taswira mbaya kwa jamii.
“Mwaka huu tunatangaza mapema kuwa kama fedha za kwenda kwenye mafunzo kwa vitendo(field) hazitakuwepo nasi hatutaenda,” alisema Venanc

Aidha alisema viongozi wengi walioko madarakani wanatumia vibaya nyazifa na fedha zao kuwalaghai wanafunzi wa kike nao kwa shida walizonazo wanajikuta wakiingia kwenye mitego hiyo.
“Tunawaona wanavyokuja na mashangingi yao kuwalaghai dada zetu huku hawawatekelezei madai yao wawalipe kwa wakati ili wasije wakaingia vishawishini,” alisema Venance.
Alisema anamkumbusha Waziri Mkuu Mizengo Pinda kauli yake aliyoitoa mwaka 2010 kuwa fedha za kujikimu zitakuwa zinapanda kila baada ya miaka mitatu kwani toka kipindi hicho mpaka sasa haijawahi kupanda.
“Tangu Waziri Mkuu aliposema kuwa watakuwa wanafanya tathmini na kupandisha fedha za kujikimu mpaka leo haijawahi kupanda japo gharama za maisha zinapanda kila siku,” alisema
Alipotafutwa, Msemaji wa Bodi ya Mikopo, Cosmas Mwaisobwa alisema madai ya wanafunzi wa vyuo vyote yameanza kushughulikiwa kwa kuanza na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

No comments:

Post a Comment