Wednesday, May 20, 2015

JESHI LA POLISI LAWAMANI KUWADHARIRISHA WANACHAMA CUF





TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), imetoa ripoti yake ya uchunguzi dhidi ya tuhuma kwa Jeshi la Polisi za kuwapiga na kuwadhalilisha viongozi na wafuasi wa Chama cha Wananchi (CUF), na kusema jeshi hilo lilitumia nguvu kupita kiasi na kuwadhalilisha wanawake wawili wa chama hicho.
Akitoa ripoti hiyo jana jijini Dar es Salaam kwa waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Bahame Nyanduga alisema pia jeshi hilo lilikiuka misingi ya Utawala Bora kwa wana CUF  katika tukio lililotokea eneo la Mtoni Mtongani wakati wanachama hao wakienda kuahirisha mkutano wao Mbagala Zakhem.
Nyanduga alisema tukio hilo la ukiukwaji wa  haki za binadamu lilitokea Januari 27,mwaka huu ambapo taarifa zilionyesha kuwa polisi hao waliwapiga na kuwakamata wananchi waliokuwa kwenye msafara wa Mwenyekiti wa CUF, Ibrahim Lipumba.
Alisema mambo yaliyobainika katika uchunguzi huo ni polisi kutumia nguvu kupita kiasi na kusababisha majeraha kwa viongozi wa CUF, kuathiri baadhi ya raia maeneo ya jirani na kukiuka misingi ya utawala bora kwa kutokuheshimu haki za binadamu.
“Tukio lile tume yetu pia ilibaini lilikuwa na udhalilishaji dhidi ya wanawake wawili wa CUF wakati wakikamatwa na kupelekwa mahabusu gereza la Segerea,”alisema Nyanduga.
Alisema kutokana na uchunguzi huo na matokeo ya ripoti hiyo tume imetoa mapendekezo kwa taasisi mbalimbali za serikali na vyama vya siasa kwa jeshi la polisi.
Alisema miongoni mwa mapendekezo hayo ni pamoja na kuzingatia kanuni, sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku, kutoa mafunzo kwa askari wake wanaoratibu shughuli za maandamano ya raia au vyama vya siasa.
Mengine ni kuhakikisha askari na maafisa wake wanapatiwa mafunzo ya mara kwa mara yahusuyo haki za binadamu na misingi ya utawala bora.
 pia katika operesheni zake lifuate utaratibu na kanuni za jeshi kwa kuzingatia jinsia za watumiwa na askari wanao washughulikia.
Wakati huohuo, Tume imetoa angalizo kwa polisi kuzingatia uhuru wa vyombo vya habari wakati wa utekelezaji wa operesheni zake na jeshi la Magereza lisitishe mara moja kufanya upekuzi wa watuhumiwa na kuepuka udhalilishaji wa heshima na utu wa binadamu.
Pia tume hiyo imekitaka chama cha CUF kutafuta namna ya kuboresha mahusiano na polisi ili kuepuka mivutano isiyo na tija katika shughuli za kisiasa, kuepusha vurugu na kulinda haki za binadamu.
“CUF  ilikiri kumiliki kikundi cha ulinzi cha Blue Guard hivyo tunakiomba kuzingatia katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inayozuia chama cha siasa kuwa na  kikundi cha mtazamo wa aina hiyo.

No comments:

Post a Comment